البحث

Majadiliano ya Kidini na Kesi ya Palestina katika Moyo wa Shughuli za Udhamini wa Nasser

2025/05/26

Jukwaa la Nasser la Kimataifa lilitangaza kuandaa ziara katika Kanisa Kuu la Al-Markasiya huko Abbasiya kama sehemu ya uzinduzi wa shughuli za siku ya kumi na nne za toleo la tano la Udhamini wa Nasser kwa Uongozi wa Kimataifa, unaoandaliwa chini ya Ufadhili wa Mheshimiwa Rais Abdel Fattah El-Sisi, na kwa ushirikiano na Umoja wa Mataifa. Ziara hiyo iliwahusisha takriban vijana 150 wa kike na wa kiume kutoka nchi mbalimbali duniani, wakiwa ni viongozi vijana kutoka sekta tofauti za kiutendaji, pamoja na vijana wenye ushawishi mkubwa katika jamii zao.

Mheshimiwa Papa Tawadros II, Papa wa Alexandria na Patriaki wa Kanisa la Al-Markasiya, aliwapokea Dkt. Ashraf Sobhy, Waziri wa Vijana na Michezo, viongozi kadhaa wa wizara, pamoja na ujumbe wa vijana washiriki wa toleo la tano la Udhamini wa Nasser kwa ajili ya ziara yao katika kanisa hilo. 

Kwa upande wake, Papa Tawadros II aliwakaribisha vijana hao kwa furaha kubwa, akieleza kufurahishwa kwake na uwepo wao unaoakisi roho ya vijana wa dunia na utofauti wa kitamaduni. Alisifu juhudi kama hizi ambazo huchangia kujenga madaraja ya uelewano kati ya mataifa, na kusisitiza umuhimu wa nafasi ya vijana katika kukuza maadili ya kuishi pamoja kwa amani na kuvumiliana.

Dkt. Ashraf Sobhy, Waziri wa Vijana na Michezo, alisifu nafasi ya Kanisa la Kikoptiki katika kukuza mshikamano wa kijamii, na akaelezea kuvutiwa kwake na shughuli zinazofanywa na kanisa kwa ajili ya kuongeza uelewa wa vijana kuhusu historia na urithi wao. Alieleza kuwa wizara yake inaendesha programu mbalimbali kwa ajili ya kuwawezesha vijana katika nyanja kama vile uongozi, uelewa wa kitamaduni na ushiriki wa kijamii. Pia alisisitiza umuhimu wa kushirikiana na taasisi mbalimbali katika kukuza mshikamano wa kijamii na utamaduni wa majadiliano na kuishi kwa amani pamoja.

Papa Tawadros II alitoa muhtasari mpana kuhusu Kanisa la Kikoptiki la Kiorthodoksi na historia yake, akilitaja kuwa miongoni mwa makanisa ya kale zaidi na ya heshima kubwa katika Mashariki ya Kati. Alifafanua kuwa Kanisa hilo lina nafasi ya kipekee kama chombo kikubwa zaidi cha wananchi nchini Misri, likiwa limeanzishwa na Mtakatifu Marko katika karne ya kwanza ya Milenia. Papa alieleza kuwa hadi leo, kanisa linaendelea kudumisha ujumbe wake wa kiroho na wa kitaifa chini ya uongozi wake kama Papa wa 118 katika mfululizo wa mapapa wa Kanisa hilo. Alielezea pia mchango wa kijamii wa Kanisa la Kikoptiki ndani na nje ya Misri kupitia huduma mbalimbali na ofisi maalum ya miradi ya kijamii kwa Wamisri wote. Kanisa hilo linaendesha shule, miradi ya maendeleo, elimu, afya, na mengineyo, pamoja na kuendeleza uhusiano mzuri na madhehebu mengine ya Kikristo.

Katika hotuba yake kwa washiriki wa toleo la tano la Udhamini wa Nasser kwa Uongozi wa Kimataifa, Papa Tawadros II aligusia vipengele vya kijiografia na kitamaduni vya Misri, akisisitiza nafasi ya kipekee ya nchi hiyo kati ya mabara matatu, na urithi wake wa kihistoria unaotokana na ustaarabu saba mfululizo. Alizungumzia pia kuhusu Mto Nile unaoashiria amani na mshikamano kati ya mataifa, na nafasi ya Misri katika maandiko matakatifu, akibainisha kuwa jina la Misri limetajwa mara 704 katika Biblia.

Papa alisisitiza kwamba Misri imekuwa chanzo cha elimu, dini, na utofauti wa kitamaduni tangu enzi za kale. Alieleza kuwa Kanisa la Kikoptiki limekuwa na nafasi muhimu katika kuhifadhi utambulisho wa taifa la Misri, sio tu kwa upande wa kiroho bali pia kwa utamaduni na uzalendo. Alikumbusha kuhusu mchango wa kanisa hilo katika kusambaza Ukristo barani Afrika, kuanzisha shule ya kwanza ya teolojia mjini Alexandria, na kutoa mfumo wa utawa kwa dunia kupitia Mtakatifu Antoni wa Jangwani, anayechukuliwa kama mtawa wa kwanza katika historia, jambo lililolifanya Kanisa la Kikoptiki kuwa rejea ya kimataifa katika maisha ya kiroho.

Papa Tawadros II aliwaeleza washiriki wa Udhamini wa Nasser kuwa upendo ni hitaji la msingi kwa kila binadamu, na ndiyo ngao madhubuti dhidi ya chuki na migawanyiko, akinukuu kauli isemayo: "Upendo hauanguki kamwe." Alisisitiza umuhimu wa kufunguka kwa wengine na kuheshimu utofauti wa mawazo na tamaduni. Pia alisifu nafasi ya Kanisa katika kuendeleza mazungumzo na ushirikiano kati ya dini na tamaduni, akisema kuwa njia hiyo ni muhimu katika kukabiliana na changamoto za sasa zinazowakabili vizazi vipya, ikiwa ni pamoja na ukosefu wa imani ya kidini, upotovu wa maadili, na usambazaji wa taarifa potofu kupitia mitandao ya kijamii. Alihitimisha kwa kusema kuwa kushikamana na maadili ya kiroho na elimu sahihi ni njia bora zaidi ya kukabiliana na changamoto hizi na kujenga jamii imara inayojikita katika upendo na uelewano wa pamoja.

Katika hitimisho la mkutano wake na washiriki wa toleo la tano la Udhamini wa Nasser kwa Uongozi wa Kimataifa Papa Tawadros II alifungua mazungumzo ya moja kwa moja na vijana waliokuwepo, waliopata fursa ya kuuliza maswali na kujadili masuala mbalimbali kwa njia ya wazi na ya ushirikiano. Ziara hiyo ilihitimishwa kwa kufanya matembezi ndani ya Kanisa Kuu la Al-Markasiya, linalochukuliwa kuwa moja ya alama kuu za Kanisa la Kikoptiki la Kiorthodoksi, kutokana na uzito wake wa kiroho na kihistoria.

Kwa upande wake, Hassan Ghazaly, Mwanzilishi wa Jukwaa la Nasser la Kimataifa, alieleza kuwa ziara ya washiriki wa programu ya ushirika katika Kanisa la Kikoptiki la Kiorthodoksi na kukutana kwao na Baba Mtakatifu Tawadros II ni hatua muhimu sana katika mchakato wa programu hiyo, kwa kuwa inaashiria kwa nguvu kubwa hali ya uwepo wa dini na tamaduni mbalimbali zinazolitambulisha jamii ya Misri. Alisisitiza kuwa mkutano huo unaakisi taswira halisi ya Misri kama nchi ya utofauti na maelewano, akibainisha kuwa kusikiliza kwao hotuba ya Baba Mtakatifu kulikuwa fursa ya kipekee ya kuelewa nafasi ya kitaifa na kiroho inayochezwa na Kanisa la Kikoptiki, pamoja na historia yake ndefu katika kuhudumia binadamu na jamii. Ghazaly aliongeza kuwa ziara hii inaimarisha maadili ya mazungumzo na uelewano kati ya dini na tamaduni mbalimbali, na inachangia katika kujenga ufahamu miongoni mwa vijana unaowawezesha kukabiliana na hotuba za chuki na mitazamo ya kibaguzi, sambamba na malengo ya ushirika katika kuandaa kizazi cha viongozi wa kimataifa wanaoamini katika amani, kuishi pamoja, na kuthamini utofauti.

"Jukwaa la Nasser la Kimataifa": Kuandaliwa kwa ziara ya washiriki wa toleo la tano la Udhamini wa Nasser kwa Uongozi wa Kimataifa katika Makao Makuu ya Al-Azhar na Kituo cha Al-Azhar cha Kupambana na Itikadi Kali, kama sehemu ya shughuli za siku ya kumi na nne ya programu.

Jukwaa la Nasser la Kimataifa lilieleza katika taarifa yake kuwa washiriki wa toleo la tano la Udhamini wa Nasser kwa Uongozi wa Kimataifa walifanya pia ziara katika Makao Makuu ya Al-Azhar na Kituo cha Al-Azhar cha Kupambana na Itikadi Kali, kama sehemu ya ratiba ya siku ya kumi na nne ya programu. Ziara hiyo ilifanyika katika muktadha wa ziara ya kielimu inayolenga kuwafahamisha vijana kutoka mataifa mbalimbali kuhusu taasisi za taifa la Misri na nafasi yake katika kujenga jamii na kueneza maadili ya amani na kuvumiliana.

Ziara hiyo ilihudhuriwa na Dkt. Muhammad Al-Dhawiny, Naibu Mkuu wa Al-Azhar, Dkt. Mahmoud Al-Hawari, Msaidizi wa Katibu Mkuu wa Baraza la Utafiti wa Kiislamu, Luteni Jenerali Ismail Al-Far, Msaidizi Mkuu wa Waziri wa Vijana na Michezo anayeshughulikia masuala ya vijana na mahusiano ya kiserikali, Alaa Eldin Al-Dessouki, Naibu Waziri na Mkuu wa Idara Kuu ya Maendeleo ya Vijana, pamoja na Reda Safina, Mkurugenzi Mkuu wa Programu za Kujitolea na Skauti, sambamba na viongozi wengine kadhaa wa Wizara ya Vijana na Michezo. Vijana walipokelewa na Mheshimiwa Dkt. Muhammad Al-Dhawiny, Naibu Mkuu wa Al-Azhar,  aliyewakaribisha washiriki wa toleo la tano la Udhamini wa Nasser kwa moyo mkunjufu, akieleza furaha yake kwa ziara hiyo inayoonesha shauku ya vijana kutoka mataifa mbalimbali kutaka kujifunza kwa karibu kuhusu taasisi kongwe za kidini nchini Misri.

Katika hotuba yake, Dkt. Al-Dhawiny alisisitiza kuwa Al-Azhar inafuata njia ya wastani na ya kati,  inayoakisi kiini cha Uislamu wa kweli – unaohimiza amani, maadili ya kibinadamu, utaifa, na mazungumzo kama msingi wa kuishi kwa pamoja baina ya wanadamu. Alieleza kuwa misingi hii ndiyo kiini cha ujumbe wa Uislamu, ambao hautofautishi watu kwa misingi yoyote, bali unasisitiza haki za binadamu wote, ikiwemo haki ya kuamini wanavyotaka.

Aidha, alifafanua kuwa Al-Azhar inaendeleza mwelekeo huu katika wito, shughuli na mahusiano yake, iwe katika ngazi ya kitaifa au kimataifa. Aligusia pia uzoefu wa "Nyumba ya Familia ya Misri", taasisi iliyoundwa kwa ushirikiano kati ya Imam Mkuu wa Al-Azhar, Dkt. Ahmed Al-Tayyeb, na Baba Mtakatifu Tawadros II wa Kanisa la Kikoptiki, ambayo inajumuisha wawakilishi wa dini ya Kiislamu na Kikristo. Taasisi hiyo imepata mafanikio makubwa nchini Misri, ikiwa imefungua zaidi ya matawi 15 katika majimbo mbalimbali ili kuendesha mashauriano na mafunzo ya pamoja, jambo linalosaidia kuimarisha maadili ya kuishi kwa amani na maelewano katika jamii.

Wakati wa kikao hicho, Mheshimiwa Dkt. Muhammad Al-Dhawiny alieleza juhudi za Al-Azhar katika kueneza maadili ya amani na kuishi kwa pamoja, akisisitiza nafasi ya kimataifa ya taasisi hiyo katika kupambana na fikra potofu kupitia elimu, wito wa kidini, na mazungumzo na wengine. Alibainisha kuwa Al-Azhar inaendelea kutekeleza ujumbe wake adhimu kupitia wahitimu wake waliotapakaa duniani kote, wanaoendeleza misingi ya wastani na msimamo wa kati. Aidha, alitaja kuwepo kwa vituo vya utafiti vilivyo chini ya Al-Azhar vinavyofuatilia na kuchambua mienendo ya kifikra iliyo potofu na kukabiliana nayo kwa kutumia elimu na hoja makini.

Naibu Mkuu huyo wa Al-Azhar alitaja pia "Hati ya Udugu wa Kibinadamu" kama waraka wa kihistoria wa kwanza uliojadiliwa na kutiwa saini na Imam Mkuu Dkt. Ahmed Al-Tayyeb na Baba Mtakatifu wa Kanisa Katoliki, ambayo ni mojawapo ya nyaraka muhimu zaidi katika enzi ya kisasa. Umoja wa Mataifa umeitambua hati hiyo kama rejea ya msingi ya kukuza maadili ya kibinadamu, haki za wanawake na wazee, na kusisitiza heshima ya binadamu bila ubaguzi. Mnamo tarehe Februari 4 – siku ya kutiwa saini kwa hati hiyo – imetangazwa kuwa Siku ya Kimataifa ya Udugu wa Kibinadamu inayoadhimishwa kila mwaka ili kuthibitisha umuhimu wa mazungumzo ya pamoja na kufanikisha amani halisi miongoni mwa mataifa.

Dkt. Al-Dhawiny aliongeza kuwa Kituo cha Kimataifa cha Al-Azhar cha Ufuatiliaji na Fatwa Mtandaoni kilianzishwa mwaka 2016 kama moja ya nguzo mpya za Al-Azhar katika kukabiliana na changamoto za kifikra na kidini duniani, kwa kufuatilia, kuchambua na kujibu kwa njia ya kielimu na kitaalamu. Alieleza kuwa wanafunzi wa Al-Azhar wanatoka katika mataifa zaidi ya 120, wakiwa zaidi ya 60,000, na wanasomea taaluma mbalimbali ikiwemo masomo ya dini, uhandisi, tiba, astronomia, hisabati na nyinginezo – jambo linalodhihirisha upeo na wigo mpana wa taasisi hiyo. Aidha, alisisitiza kuwa Chuo Kikuu cha Al-Azhar – kilicho kongwe zaidi duniani – kimezalisha viongozi wengi mashuhuri, wakiwemo marais wa nchi, mawaziri, na wanafikra, wameotoa mchango mkubwa kwa jamii zao na ubinadamu kwa ujumla, jambo linaloonyesha nafasi ya Al-Azhar kama taasisi ya elimu na kiroho ya kimataifa.

Ziara hiyo ilihusisha pia matembezi ya vijana washiriki wa toleo la tano la Udhamini wa Nasser kwa Uongozi wa Kimataifa ndani ya Kituo cha Al-Azhar cha Ufuatiliaji na Fatwa Mtandaoni pamoja na Kituo cha Al-Azhar cha Kupambana na Itikadi Kali. Washiriki walijionea kwa karibu mbinu za kazi katika vituo hivyo ambavyo ni nguzo kuu katika juhudi za Al-Azhar za kupambana na itikadi kali na kueneza uelewa sahihi wa dini. Walifahamu kuhusu Kituo cha Kupambana na Itikadi Kali cha Al-Azhar, kilichoanzishwa mwaka 2015 kwa agizo la Imam Mkuu Dkt. Ahmed Al-Tayyeb, ambacho hurekebisha dhana potofu na kujibu hotuba zenye misimamo mikali kwa kutumia njia sahihi za kielimu na kidini. Kituo hicho huchapisha kwa lugha 13 tofauti ili kuwafikia Waislamu wengi zaidi kote duniani. Washiriki pia walielezwa kuhusu idara maalumu ndani ya kituo hicho, ikiwa ni pamoja na Idara ya Fatwa kwa Wanawake, Kitengo cha “Lamm Al-Shaml” kinachoshughulika na masuala ya migogoro ya kifamilia na talaka katika jamii ya Misri, pamoja na Kitengo cha “Bayan” kinachokabiliana na mitazamo isiyo ya kidini na mitazamo ya kifikra iliyopotoka.

Katika ziara hiyo, washiriki walipata pia nafasi ya kutazama machapisho mbalimbali ya kielimu yanayotolewa na kituo hicho – kutoka majarida, kozi za mafunzo, ripoti, hadi warsha na makongamano ya uelimishaji. Mwishoni mwa ziara hiyo, kulitolewa fursa kwa washiriki kujadili na kuuliza maswali, ambapo walionesha kuelimika na kuvutiwa na maudhui yaliyowasilishwa na njia za kazi zinazotumiwa. Maswali yao yalidhihirisha ufahamu wao wa kina na mshikamano na masuala ya fikra na itikadi kali. Walitaka kujua kuhusu mbinu za ufuatiliaji na uchambuzi wa hotuba zenye misimamo mikali kwa lugha mbalimbali, na namna ya kuwasiliana na tamaduni tofauti bila kuvunja misingi ya imani. Majadiliano haya yalikuwa jukwaa muhimu la maingiliano ya kielimu na kiutamaduni lililochangia kuimarisha uelewa wa pamoja na kuthamini nafasi ya taasisi za kidini katika kukabiliana na changamoto za fikra zinazokumba jamii za kisasa.

Kwa upande wake, Hassan Ghazaly – Mwanzilishi wa Jukwaa la Nasser la Kimataifa na Mratibu Mkuu wa Udhamini wa Nasser kwa Uongozi wa Kimataifa – alisema kuwa ziara ya Kituo cha Al-Azhar cha Kupambana na Itikadi Kali na Kituo cha Fatwa Mtandaoni ilikuwa hatua muhimu katika mtaala wa kielimu wa programu ya ushirika. Alibainisha kuwa ziara hiyo iliwapa vijana nafasi ya kipekee ya kuona kwa karibu juhudi za taasisi kongwe ya kidini kama Al-Azhar katika kukabiliana na fikra potofu na kueneza maadili ya amani, wastani na kuishi kwa pamoja kati ya mataifa.

Ghazaly aliongeza kuwa kituo hicho ni mfano bora wa matumizi ya zana za kisasa katika kupambana na mawazo yenye misimamo mikali kwa lugha nyingi, jambo linaloonesha jitihada za Al-Azhar za kuwasiliana na dunia kwa lugha inayofahamika na wote. Alisisitiza kuwa ziara hiyo imewapa vijana mwamko mkubwa kuhusu masuala ya fikra, na kuonesha nafasi ya Misri katika kujenga hotuba ya kidini iliyosawazika, yenye uwezo wa kukabiliana na changamoto za fikra na utamaduni za kisasa ndani na nje ya nchi.


Udhamini wa Nasser kwa Uongozi wa Kimataifa wajadili "Kesi ya Palestina: Mtazamo na Tathmini" katika shughuli za siku ya kumi na nne kwa ushiriki wa vijana 150 kutoka nchi 80

Mwishoni mwa taarifa yake, Jukwaa la Nasser la Kimataifa lilieleza kuwa shughuli za siku ya kumi na nne za toleo la tano la Udhamini wa Nasser kwa Uongozi wa Kimataifa zilihitimishwa kwa kuandaliwa kwa kikao cha majadiliano kilichobeba kichwa: “Kesi ya Palestina: Mtazamo na Tathmini.” Kikao hicho kilimkaribisha Dkt. Saeed Abu Ali, Naibu Katibu Mkuu wa Jumuiya ya Nchi za Kiarabu na Mkuu wa Sekta ya Palestina na Ardhi Zilizokaliwa, Dkt. Yasmin Mosi, Mshauri wa Kisheria wa Wizara ya Mambo ya Nje ya Misri, na Sahar Al-Jubouri, Mkuu wa Ofisi ya Mwakilishi wa UNRWA jijini Kairo. Kikao kiliendeshwa na Sharif Jad, Mkurugenzi wa shughuli za kitamaduni katika Kituo cha Utamaduni cha Urusi na Balozi wa Elimu na Sayansi wa Shirikisho la Urusi, kwa kuhudhuriwa na Alaa Eldin El-Dessouky, Naibu Waziri na Mkuu wa Idara Kuu ya Maendeleo ya Vijana, pamoja na Hassan Ghazaly, Mwanzilishi wa Jukwaa la Nasser la Kimataifa, na viongozi kadhaa kutoka Wizara ya Vijana na Michezo.

Sharif Gad, Mkurugenzi wa shughuli za kitamaduni katika Kituo cha Urusi, alieleza furaha yake kwa kuwepo miongoni mwa vijana kutoka mataifa mbalimbali, akisisitiza kuwa vijana wa dunia ndio viongozi wa baadaye, wenye uwezo wa kuleta mabadiliko ya maendeleo katika nchi zao na kusambaza fikra za mwanga na maelewano kati ya mataifa. Alitoa salamu za heshima kwa watu wote wanaoiunga mkono Kesi ya Palestina, akieleza shukrani zake kwa kamati ya maandalizi kwa kumchagua kuhudhuria kikao hiki muhimu. Alisisitiza kuwa Palestina ni kesi ya muda mrefu inayodumu vizazi kwa vizazi. Alibainisha kuwa majadiliano yanaweza kuchukuliwa kwa mtazamo wa kukatishwa tamaa au wa matumaini, na yeye anaunga mkono mtazamo wa matumaini. 

Aidha, alieleza heshima yake kubwa kwa watu wa Misri ambao wameendelea kukataa wazi wazi suala la kuanzisha uhusiano wa kawaida na Israel, akisema kuwa hali hiyo haionekani kwa dhahiri mitaani mwao kama ilivyo katika baadhi ya nchi nyingine za Kiarabu. Aliongeza kuwa serikali ya Misri inaelewa vyema suala hili, na watu wake hawatakubali hali ya kawaida hadi pale ambapo dola huru ya Palestina itakapoundwa. Alihitimisha kwa matumaini licha ya changamoto zinazokabili Kesi ya Palestina, akiwapongeza Wapalestina kwa kusimama kidete dhidi ya uhamishaji wa lazima, na kuipongeza Misri na viongozi wake kwa msimamo wao wa wazi wa kuukataa uhamishaji huo, akisisitiza kuwa Palestina itaendelea kuwepo hadi dola huru ya Palestina itakapopatikana.

Dkt. Saeed Abu Ali, Naibu Katibu Mkuu wa Jumuiya ya Nchi za Kiarabu, aliwakaribisha vijana waliokuwa wakishiriki na kutoa shukrani zake na pongezi kwa Waziri wa Vijana na Michezo wa Misri kwa mwaliko wake wa kushiriki katika toleo hili la Ufadhili wa Nasser wa Uongozi wa Kimataifa, ambao alikubali kwa heshima kwa Waziri huyo, kwa upendo kwa vijana, na kwa kuzingatia umuhimu wa tukio hili. Alisisitiza kuwa toleo hili linabeba jina la kiongozi wa kipekee, Gamal Abdel Nasser, ambaye, licha ya kufariki, bado yuko hai katika nafsi za watu wa mataifa haya na akili za viongozi wao, tukimkumbuka kwa heshima na dua kwa roho yake safi. Aliongeza kuwa pamoja naye tunawakumbuka viongozi wengine waliotangulia, waliotukuka kwa juhudi zao za kupigania amani na haki, kama vile Nehru, Gandhi, na viongozi wote waliokuwa sauti ya nchi za Kusini na waliosimamia harakati za ukombozi na maendeleo katika mazingira ya usawa na haki. Viongozi hao walianzisha pamoja Harakati ya Kutofungamana na Upande Wowote. Alihitimisha hotuba yake kwa kusema: “Ninyi vijana mnaalikwa leo kubeba bendera ya misingi hiyo ya heshima na kuendeleza harakati hizo.”

Katika hotuba yake, Dkt. Saeed Abu Ali alitoa shukrani za dhati na pongezi kubwa kwa Misri, akilisifu jukumu lake muhimu na juhudi zake zinazoendelea, akimtaja Rais Abdel Fattah El-Sisi kama kinara wa juhudi hizo, ameyeendeleza uzoefu huu wa kipekee unaobeba jina lenye thamani kubwa kwa umma wa Kiarabu. Alisisitiza nafasi ya juu ambayo Misri inashikilia duniani, kwani inabeba dhamana yake ya kihistoria na kutekeleza wajibu wake katika kuleta utulivu na maendeleo, huku ikiendeleza jukumu lake la msingi la kulinda na kuimarisha misingi ya haki. Aliongeza kuwa leo hii Misri inaendeleza mafanikio haya makubwa, akiishukuru kwa jukumu lake muhimu na la kuamua katika mazingira ya sasa, kwa kutetea masuala ya umma wa Kiarabu, kulinda wananchi wa Palestina, na kuendeleza msaada wake wa kihistoria kwa harakati zao halali. Alifafanua kuwa msaada huo unaakisi ujumbe wa kudumu wa Misri katika kutetea maadili ya uhuru, haki, na amani, hasa ikizingatiwa hali ya sasa ya vita ya kichaa na mauaji ya kimbari dhidi ya watu wa Palestina, hususan katika Ukanda wa Gaza, hali inayodhihirisha mateso ya kihistoria wanayopitia kwa zaidi ya karne moja.

Katibu Msaidizi Mkuu wa Jumuiya ya Nchi za Kiarabu alitoa muhtasari wa historia ya suala la Palestina, akieleza kuhusu harakati ndefu na endelevu za wananchi wa Palestina kwa miongo kadhaa hadi kufikia matukio ya hivi karibuni, yaliyoshuhudia ongezeko kubwa la mashambulizi ya Israeli, yaliyopelekea idadi kubwa ya mashahidi, huku kukiwa na mlengo wa makusudi wa kuwalenga watoto na wanawake, kama njia ya kimkakati ya kutokomeza uwepo wa Wapalestina. Alisema kuwa uvamizi huo unatumia mbinu mbalimbali za kuwahamisha kwa nguvu, zikiwemo njaa, kiu, kuzuia matibabu, pamoja na uharibifu wa miundombinu ya kibinadamu, kidini na kielimu, ikiwemo makanisa, misikiti, shule na vyuo vikuu. Aliongeza kuwa Nakba (Janga la Palestina) inajirudia leo kwa sura zilezile za zamani, lakini sasa inatangazwa moja kwa moja kwenye runinga mbele ya macho ya dunia nzima. Katika muktadha huu, utawala wa Israeli unajaribu kunyamazisha sauti zinazofichua ukweli kwa kuwalenga waandishi wa habari, ambapo zaidi ya waandishi 200 wameuawa tangu kuanza kwa matukio ya hivi karibuni – jinai inayolenga kufuta ukweli na kuzuia mateso ya wananchi wa Palestina yasijulikane ulimwenguni.

Dkt. Saeed Abu Ali alijiuliza: ni hatua gani zinahitajika kuchukuliwa katika ngazi ya Kiarabu na kimataifa kukabiliana na jinai hii inayoendelea? Akasisitiza kuwa sasa dunia inakabiliwa na unyama wa hali ya juu na ukiukaji mkubwa wa haki za binadamu, kana kwamba kuna jaribio la kuurudisha ubinadamu katika sheria za msituni, kwa kupuuza kabisa maadili ya kibinadamu na kubomoa mafanikio ya kihistoria ya sheria za kimataifa zilizowekwa ili kudumisha amani na usalama duniani. Alieleza kuwa jinai ya mauaji ya kimbari sasa haijabaki Gaza pekee, bali imeenea kwa sura zake zote hadi Ukingo wa Magharibi pia, na kuwa sasa ni vita kamili dhidi ya wananchi wote wa Palestina, vita vinavyotumia kila njia na zana kwa lengo la kuangamiza kabisa suala la Palestina na kuwafukuza watu hao kutoka ardhi yao. Alihitimisha kwa kusema kuwa kinachoendelea sasa ni tishio la uwepo na mustakabali wa watu wa Palestina, hali inayohitaji hatua ya haraka na madhubuti kutoka kwa jumuiya ya Kiarabu na kimataifa ili kukomesha jinai hii ya kikatili.

Aidha, Katibu Msaidizi Mkuu wa Jumuiya ya Nchi za Kiarabu alieleza kuwa ingawa kuna mwitikio wa kimataifa katika kukabiliana na kinachoendelea Palestina, bado mwitikio huo ni wa polepole. Hata hivyo, alisisitiza kuwa juhudi za Kiarabu zimeongezeka maradufu, na kuna mashauriano, shinikizo, na mawasiliano ya kuratibiwa katika ngazi za Kiarabu na kimataifa ili kusitisha vita. Alibainisha kuwa sasa kuna nchi 137 duniani zinazotambua rasmi taifa la Palestina. Alieleza kuwa vikao vitano vya kilele vimefanyika – vya mwisho vikiwa mwezi Oktoba 2023 – vikiwemo vikao viwili vya kilele vya pamoja vya Kiarabu na Kiislamu, na kikao cha dharura kilichofanyika Kairo. Vikao vyote hivi vilikubaliana juu ya madai ya msingi, likiwemo kusitisha vita, kutoa misaada ya kibinadamu ya dharura, kuachiliwa kwa mateka na wafungwa kwa njia ya pande zote mbili, kufunguliwa kwa mipaka na kumaliza mzingiro, kujiondoa kwa Israel kutoka Gaza na kukomesha udhibiti wake, pamoja na kufungua njia ya kisiasa ya kuleta haki kwa watu wa Palestina na kuwawezesha kuanzisha taifa lao huru kwa mujibu wa maazimio ya sheria za kimataifa. Alisisitiza kuwa huo ndio msingi wa kweli wa amani ya kudumu katika eneo hilo, na kwamba haiwezekani kuwa na uhusiano wa kawaida na Israel pasipo kutatuliwa kwa haki suala la Palestina. Alisisitiza kuwa watu wa Palestina bado wapo, wanaendeleza uwepo wao, na wanaendelea na mapambano yao; ni watu halisi wasiotoweka, bali wenye dhamira imara kuliko wakati wowote. Vilevile, alisisitiza kuhusu ulazima wa kuijenga upya Gaza, akieleza kuwa mpango wa Misri uliozinduliwa katika Kikao cha Cairo sasa umekuwa mpango wa nchi za Kiarabu wote, kama hatua ya vitendo ya kuijenga Gaza na kuunga mkono ustahimilivu wa watu wa Palestina.

Mkuu wa Sekta ya Palestina na Ardhi Zilizokaliwa aliwaelekeza hotuba yake kwa vijana, akisisitiza jukumu lao kuu katika nchi zao kupitia uelewa wao unaozidi kuongezeka na fursa kubwa zinazotolewa na teknolojia kwa ajili ya kuleta athari na kuunda mabadiliko. Alisema: “Ninyi ni kizazi chenye uwezo wa kuleta mabadiliko tunayoyatarajia. Tuna imani kubwa nanyi, tunawategemea, na tunawapenda na kuwathamini kwa dhati.” Alifafanua kuwa maendeleo ya kisiasa tunayoyashuhudia leo hayawezi kutenganishwa na nguzo muhimu inayoyategemeza, nayo ni jukumu la mataifa ya Kiarabu kupitia Jumuiya ya Nchi za Kiarabu, kwa kushirikiana na mashirika mbalimbali ya kikanda na kimataifa. Alitaja matarajio makubwa na juhudi zinazofanyika kwa bidii ili kuweka mfumo wa ushirikiano wa kweli na Umoja wa Ulaya ili kuunga mkono msimamo wa Kipalestina na Kiarabu. Alisisitiza kuwa msingi wa msimamo wa Kiarabu ndani ya Jumuiya ya Nchi za Kiarabu ni mpango wa Palestina, unaochukuliwa kuwa ni fremu ya kisiasa inayowakilisha matarajio ya watu wa Palestina kuelekea uhuru, kujitawala, na kuanzisha dola huru ya Palestina.

Kwa upande wake, Dkt. Yasmine Moussa, Mshauri wa Kisheria katika Wizara ya Mambo ya Nje ya Misri, alieleza shukrani zake za dhati kwa timu inayosimamia Ufadhili wa Nasser, wakati wa hotuba yake kwa washiriki wa toleo la tano la ufadhili huo. Alieleza fahari na heshima yake kwa kushiriki kwenye mkusanyiko huu mkubwa ili kujadili Kesi ya Palestina na mchango wa Wizara ya Mambo ya Nje ya Misri katika suala hilo. Alisisitiza kuwa uhusiano wa Misri na Kesi ya Palestina ni wa asili, kizazi hadi kizazi, kitamaduni na wa kiroho. Alibainisha kuwa kesi hii imeunda uelewa wa kisiasa wa vijana, na kwamba vijana wameonesha kukataa kwa dhati yanayotendeka upande wa pili. Alitarajia kwamba kikao hiki, pamoja na uelewa na mipango inayotolewa na vijana, kitakuwa na athari halisi katika kurejesha haki kwa wenyewe na kuimarisha haki katika kesi hii ya msingi. Aliongeza kuwa Wizara ya Mambo ya Nje ya Misri inachukua jukumu la kihistoria, linalotambulika na lililoandikwa katika kuunga mkono Kesi ya Palestina, jukumu ambalo linaendelea na kuimarika zaidi, hasa katika mazingira ya sasa yenye mabadiliko ya haraka.

Katika hotuba yake, Yasmine Moussa aliangazia maendeleo ya hivi karibuni katika kesi ya Palestina pamoja na juhudi za Misri katika miaka ya karibuni, hasa kuhusiana na vipengele vya kisheria vinavyohusiana na kesi hiyo. Alisisitiza mchango mkubwa na muhimu wa Misri katika suala la Palestina. Pia alizungumzia yaliyowasilishwa katika Mahakama ya Kimataifa ya Jinai (ICC) kuhusu matendo ya Israel na ukiukaji wake wa mara kwa mara, ambao hauishii tu katika uvamizi wa kijeshi, bali unajumuisha pia ukiukaji mkubwa wa sheria za kimataifa za kibinadamu. Alieleza kuwa ukiukaji huu haujakabiliwa na msimamo madhubuti wa kimataifa hadi sasa, licha ya kwamba sheria za kimataifa ni msingi muhimu katika kushughulikia masuala ya aina hiyo. Dkt. Yasmine alisisitiza umuhimu wa sheria za kimataifa na nafasi ya mashirika ya kimataifa ya kisheria katika kuunga mkono uhuru na kujitawala kwa Palestina. Alisisitiza pia umuhimu wa kutekelezwa kwa maazimio ya Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa, na kwamba ni muhimu kutolewa kwa warrants za kukamatwa kwa wale wanaohusika na uhalifu huu, akiwemo Waziri Mkuu wa Israel, ili kufanikisha mafanikio yaliyokusudiwa na kurejesha matumaini ya kufikia suluhisho la haki na usawa kwa suala la Palestina.

Kwa upande mwingine, katika hotuba yake, Sahar Al-Juboury, Mkuu wa Ofisi ya Mwakilishi wa UNRWA jijini Cairo, alielezea nafasi ya Shirika la Kuhudumia Wakimbizi wa Kipalestina (UNRWA), akieleza kuwa shirika hilo linatoa msaada, ulinzi, na huduma mbalimbali zinazohusiana na elimu, huduma za afya, na misaada ya dharura. Alifafanua kuwa UNRWA limekuwa taasisi kuu katika kutoa msaada kwa Wapalestina, hasa katika mazingira ya sasa yenye changamoto kubwa. Alibainisha kuwa ufadhili wa UNRWA unategemea michango kutoka kwa nchi wanachama wa Umoja wa Mataifa, na kwamba iwapo shirika hilo litasitisha shughuli zake, baadhi ya watu wanaamini kuwa haki za Wapalestina zitaisha, jambo ambalo ni hatari na la wasiwasi. Alieleza ukubwa wa janga la kibinadamu, akitaja kuwa idadi ya watoto waliopoteza viungo huko Gaza ni kubwa kuliko sehemu nyingine yoyote duniani. Pia alielezea juhudi za kila siku za shirika hilo, kama vile kutoa zaidi ya ushauri wa kitabibu 60,000 kila siku, na kuondoa taka kutoka katika kambi za wakimbizi, licha ya changamoto kubwa za usalama na kifedha ambazo shirika linakabiliana nazo tangu mwaka 2015.

Katika hotuba yake, Sahar Al-Juboury alisisitiza kuwa mgogoro wa sasa ni mkubwa zaidi kuwahi kukumba shirika la UNRWA, na kwamba uendelevu wa shughuli zake uko hatarini iwapo hakutapatikana ufadhili wa kutosha. Alieleza kuwa kutosaidiwa na nchi wafadhili kunazuia kwa kiasi kikubwa uwezo wa shirika hilo kuendelea kutoa huduma. Hata hivyo, alionesha shukrani kwa msaada wa kipekee kutoka kwa watu binafsi na makampuni makubwa tangu kuanza kwa vita, huku akieleza kuwa kuna jitihada za makusudi za baadhi ya pande kudhoofisha wafadhili na kupotosha ukweli, ili kufuta haki za wakimbizi wa Kipalestina. Alizungumzia hali ya sasa ya kesi ya Palestina kutoka mtazamo wa UNRWA, akifafanua kuwa watu wa Palestina wanakabiliwa na mateso na ukiukaji wa haki kila siku, na kwamba nafasi ya UNRWA bado ni ya msingi na muhimu kwa kila mkimbizi wa Kipalestina. Shirika hilo ni mhimili wa maisha yao, hasa katika mazingira magumu wanayoishi, hususan katika kambi za wakimbizi. Katika kujibu moja ya maswali, alieleza changamoto ya kukosekana kwa tafsiri ya pamoja ya dhana ya “ugaidi” katika sheria za kimataifa, akifafanua kuwa hadi sasa hakuna maana ya pamoja ya ugaidi, jambo linalotoa mwanya kwa kila nchi kufasiri dhana hiyo kulingana na sheria na sera zake za ndani. Alisisitiza kuwa kukosekana kwa tafsiri ya pamoja kunapelekea kupinduliwa kwa dhana, ambapo harakati za ukombozi wa Palestina huoneshwa kana kwamba ni uhalifu, huku wamiliki halali wa ardhi wakiwa ndio wahanga wa kweli. Katika hitimisho la hotuba yake, alielekeza ujumbe kwa vijana, akiwasihi kwamba wanaweza kuwa chachu ya mabadiliko katika jamii zao, na kwamba wanaweza kuunga mkono suala la Palestina kwa njia yoyote ile, hata kama ni ndogo, kwani kila juhudi ina mchango wake na ina maana kubwa. 

Katika hitimisho la kikao hicho, fursa ilitolewa kwa washiriki kutoa maswali na michango, ambapo waligusia hali ya sasa katika ardhi za Palestina, mwelekeo wa mabadiliko yanayoweza kutokea katika siku zijazo, na nafasi ya jumuiya ya kimataifa na ya Kiarabu katika kipindi kijacho. Mojawapo ya maswali yaliyoibuliwa lilihusu suala la uhusiano wa kawaida, ambapo ilielezwa kuwa mkataba wa amani wa Misri ulizingatia kanuni ya “ardhi badala ya amani”, ambao ndiyo msingi wa kurejesha mamlaka kamili ya Misri juu ya Sinai. Kwa hivyo, hakuna mlinganisho wowote kati ya aina hii ya mkataba na aina nyingine za ushirikiano ambazo hazihusiani na kurejesha haki au kuleta haki. Swali jingine lilihusu maana ya ugaidi, ambapo ilirudiwa kuwa hakuna tafsiri ya pamoja ya kimataifa, jambo linalosababisha mijadala mingi na tofauti za tafsiri kutoka nchi moja hadi nyingine. Kikao hicho kiliendelea zaidi ya muda uliopangwa kutokana na mwitikio mkubwa wa washiriki na mijadala ya kina. Hatimaye, picha ya pamoja ilipigwa ikiwa ni kumbukumbu ya tukio hilo lililojaa ushirikiano na hali ya uelewa mkubwa juu ya suala la Palestina.

أخبار ذات صلة: